WAZIRI
MKUU Mizengo Pinda amesema jitihada zaidi zinatakiwa kufanyika ili kuongeza
uzalishaji wa mazao ya nyuki hapa nchini na kufikia angalau asilimia 50 ya
uwezo ilionao wa kuzalisha tani 140,000 za asali na tani
10,000 za nta kwa mwaka.
“Mapori
yote nchini pamoja na maeneo ya kilimo yana uwezo mkubwa wa kuzalisha mazao ya
nyuki kwa wingi. Ushiriki wa sekta binafsi katika uzalishaji na uwekezaji
katika viwanda bado ni mdogo hivyo nahimiza na kuamini kuwa ushiriki wa sekta
binafsi ni chachu kubwa katika kukuza sekta hii ya ufugaji nyuki,” alisema.
Alitoa
kauli hiyo jana jioni (Ijumaa, Agosti 30, 2013) wakati akizungumza wahitimu,
wakufunzi na wazazi waliohudhuria mahafali ya kwanza na ya pili ya Chuo
cha Mafunzo ya Ufugaji Nyuki cha Tabora yaliyofanyika kwenye viwanja vya chuo
hicho.
Jumla
ya wanafunzi 68 wamehitimu vyeti na stashahada ikiwa ni wahitimu wa mwaka
2011/2012 na 2012/2013 tangu kurejeshwa rasmi kwa mafunzo hayo kwenye chuo
hicho cha Tabora kutoka Chuo cha misitu cha Olmotonyi kilichopo Arusha.
Waziri
Mkuu alisema katika kipindi cha miaka minne iliyopita, kuanzia mwaka 2009 hadi
2012, uzalishaji wa asali hapa nchini ulifikia wastani wa tani 8,747 na wa nta
ulifikia tani 583 kwa mwaka ambayo ni sawa na asilimia saba tu ya uwezo ambao
nchi hii inao.
Alisema
Tanzania ni moja kati ya nchi tano za Afrika zilizoruhusiwa kuuza asali yake
katika soko la Umoja wa Nchi za Ulaya. Nchi nyingine ni Ethiopia, Zambia,
Cameroon na Uganda. Alisema Ethiopia ndiyo inayoongoza kwa uzalishaji katika
Afrika ikifuatiwa na Tanzania.
“Roho
inaniuma ninaposikia kwamba Ethiopia ndiyo inaongoza kwa uzalishaji wa mazao ya
nyuki barani Afrika. Wao wana jangwa kubwa tu, sisi tuna misitu kibao na maji
ya kutosha. Lazima tujiulizie ni wapi tulikosea kwa sababu Tanzania ilikuwa
inaongoza kwa uzalishaji kwenye miaka ya 60,” alisisitiza.
Ameutaka
uongozi wa Chuo cha Mafunzo ya Ufugaji Nyuki cha Tabora pamoja na Wizara ya
Maliasili na Utalii wajipange na kuona namna ya kuinua uzalishaji huu. “Mkipata
mitambo kidogo tu ya kusindika asali mtakuwa na nafsi kubwa ya kuwa wauzaji
wakubwa wa asali nje ya nchi... wanunuzi wa nje wanataka traceability,
ni rahisi kwa chuo kufanikiwa katika hili,” alisema.
“Soko
lipo na bei nzuri. Tutumie fursa hii kuuza
mazao yetu ndani na nje ya nchi ili kuongeza kipato cha kaya na cha Taifa kwa
ujumla. Kama Asali inayozalishwa nchini itafungashwa vizuri kitaalam, kuna soko
kubwa katika miji mikubwa, mahoteli, mashirika ya ndege, migodini na kwenye
vituo vya utalii,” alisema.
Aliwataka
wahitimu wa Chuo hicho watambue kwamba mafanikio katika maisha yao
hayatategemea tu elimu ya ufugaji nyuki waliyojifunza, bali yatatokana na jinsi
watakavyoitumia elimu hiyo kwa vitendo. “Elimu yenu ni zana, ni silaha, kwa
hiyo itumieni vizuri. Ni silaha ya kuajiriwa, kujiajiri au kuwaajiri wengine
katika miradi ya ufugaji wa nyuki, uzalishaji wa asali na nta na hatimaye
kuleta maendeleo yenu binafsi na ya jamii nzima kwa ujumla,” aliwasihi.
Mapema,
akitoa salamu za Mwenyekiti wa Bodi ya Chuo hicho, Kaimu Mwenyekiti, Bw. Liana
Hassan aliiomba Serikali ikisaidie chuo hicho kupata sh. milioni 37/- ili
kiweze kukamilisha mitaala yake kwa kuzingatia vigezo vya NACTE. Alisema
kukamilika kwa hatua hiyo, kutakiwezesha chuo hicho kupata ithibati yake
mapema.
Kuhusu
changamoto zinazokikabili chuo, Bw. Hassan alisema miundombinu ya chuo
haitoshi, madarasa hayatoshi, mabweni yamechakaa, na kwamba wanahitaji vifaa
vya kisasa ili waweze kupata tarifa kupitia njia ya mtandao (internet).
Kuhusu
tatizo la usafiri, Bw. Hassan alisema chuo kina gari moja tu ambalo ni la muda
mrefu sana. “Tunaomba kupatiwa minibus mbili za wanafunzi, Land-Cruiser pick-up
mbili ili zisaidie kubeba mahema na vifaa vingine wakati wanafunzi wakienda
porini kimasomo na Land-Cruiser station wagon mbili kwa ajili ya idara ya
utawala,” alisema.
Wakati huohuo, Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Bibi Fatma Mwassa wakati akitoa
salamu za mkoa huo kwa wahitimu aliwaasa wasisubiri kazi za kuajiriwa bali
wafikirie kujiajiri kwani mafunzo waliyohitimu yanawapa fursa hiyo. Alitoa ofa
ya mizinga ya nyuki kwa vijana 10 wa kutoka Tabora watakaojiunga pamoja na
kuamua kuanzisha manzuki (apiary) yao ili kujiletea maendeleo.
No comments:
Post a Comment