Sunday, September 9, 2012

SERIKALI KUAHIDI AJIRA 1000 KWA MAAFISA MISITU.

WIZARA ya Maliasili na Utalii, inatarajia kuajiri maofisa misitu 1,000 mwaka wa fedha 2012/13 ili kupunguza uhaba wa maofisa hao nchini, hivyo kukabiliana na vitendo vya uharibifu wa mazingira.
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alitangaza neema hiyo katika mahafali ya Chuo cha Misitu Olmotonyi, wilayani Arumeru, Mkoa wa Arusha.
Nyalandu alisema tatizo la ajira kwa maofisa misitu, sasa litabaki kuwa historia hasa baada ya Serikali kuunda Wakala wa Misitu, ambao hadi sasa ikama yao inahitaji wafanyakazi 2,500.
“Serikali inathamini zaidi taaluma ya maofisa misitu, kwani ni muhimu katika suala zima la utunzaji na uhifadhi wa misitu iliyopo nchini, ili kulinda Tanzania isiwe jangwa, ajira za maofisa misitu zilikuwa zimesimamishwa sambamba na ajira nyingine, lakini sasa zimerejeshwa,” alisema Nyalandu.
Alisema hivi sasa hekta 90,000 za misitu ya uoto wa asili zinapotea kila mwaka kutokana na ujangili wa misitu, biashara ya kuchoma mkaa na kuvunwa bila utaratibu.
 “Hivyo, ili kukabiliana na changamoto hizi, Serikali inahitaji kuwa na maofisa misitu wa kutosha na tutawaajiri wahitimu wote 121 wa mwaka huu katika chuo hiki. Pia, tutawahitaji wahitimu 107 wa mwaka jana na hata 101 wa mwaka juzi, wengine waliokuwa hawana ajira,” alisema Nyalandu.
Kuhusu matatizo ya chuo hicho, Nyalandu alisema wizara itajitahidi kuyafanyia kazi, ikiwamo kurekebisha mfumo wa uongozi hivyo kukipa fursa ya kujiendesha na kuajiri walimu wake, ili kiweze kupandisha madaraja kwa walimu na watumishi wengine kama vilivyo vyuo vingine.
Hata hivyo, Nyalandu aliwataka wahitimu hao kutumia taaluma hiyo vyema na kulisaidia taifa kukabiliana na changamoto za mazingira, hivyo kuwa mabalozi wazuri wa chuo hicho katika soko la ajira.
Awali, Mkuu wa chuo hicho, Christogunus Haule alisema wanatoa mafunzo ya cheti na stashahada ya masitu, lakini kinakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwamo uchakavu wa majengo, upungufu wa walimu, bajeti isiyokidhi na na kuendesha propramu mbalimbali.

No comments:

Post a Comment